Thursday 26 April 2018

KATIKATI YA SHIDA UNAYOPITIA MUNGU YUPO

BWANA YESU ASIFIWE

Kwa uweza na nguvu itokayo juu Leo nakuletea somo lenye kichwa kinachosema, 

KATIKATI YA SHIDA UNAYOPITIA MUNGU YUPO. 

Ni kweli kabisa kuna changamoto zinazoweza kukutokea mpaka zikajaribu kuiondoa imani yako. 
Wakati mwingine unaweza ukajaribu hata kumkana Mungu lakini nakuambia hapo hapo ulipo na shida unazoziona bado Mungu amekushika mkono. 

Kwakuwa tu shetani ni baba wa uongo basi anakudanganya kwamba hili jambo haliwezekani ili uiache imani, na zaidi huwa anakutishia juu ya muda na urefu wa kukaa kwa hiyo changamoto ndani yako. 

NENO LA MSINGI

1WATHESOLONIKE 5:18
Shukuruni kwa kila jambo; maana hayo ni mapenzi ya Mungu kwenu katika Kristo Yesu.

*****************
Jambo lolote gumu linapokutokea huna budi kumshukuru Mungu maana mengine ni njia ya kukufikisha katika ndoto zako. 
Lile tatizo ni fursa kwako hivyo inabidi ulifurahie na utazamie ushindi mbele kwa kuwa mwaminifu na Mungu. 

1WAKORINTHO 10:13
Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.

***************
Kwanza utakapopatwa na changamoto amini Mungu ndiye aliyeruhusu hiyo changamoto ije kwako hivyo ni lazima yuko katikati ya hiyo changamoto. 
Mungu ni mwaminifu na ameshasema kwamba hatamuacha shetani akujaribu zaidi ya kiwango cha imani yako. 

Hapo kwenye hilo jaribu Mungu yupo na shetani pia yupo. 
Shetani yupo kwaajili ya kukupepeta akili yako ili ajue kama bado wewe ni wakwake au la. 
Na Mungu anakujuwa kwamba wewe ni wakwake ila tu nae anakuwa pale kumthibiti shetani asije akakutwisha mzigo usio saizi yako halafu akakuiba kutoka katika ufalme wake. 

HIVYO KATIKA SHIDA YAKO MUNGU YUKO KARIBU SANA NA WEWE NA PIA SHETANI YUKO KARIBU SANA NA WEWE. 

Cha kufanya ni wewe kuwa mwaminifu ili Mungu atukuzwe na uwe na ushuhuda uliokamilika kisha akujivunie. 

AYUBU 1:9-12
Ndipo Shetani akamjibu BWANA, na kusema, Je! Huyo Ayubu yuamcha BWANA bure?

Wewe hukumzingira kwa ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo? Kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali yake imeongezeka katika nchi.

Lakini nyosha mkono wako sasa, uyaguse hayo yote aliyo nayo, naye atakukufuru mbele za uso wako.

BWANA akamwambia Shetani, Tazama, yote aliyo nayo yamo katika uwezo wako; lakini usinyoshe mkono wako juu yake yeye mwenyewe. Basi Shetani akatoka mbele za uso wa BWANA.

*****************
Kumbe huwezi kupatwa na changamoto kama Mungu hajaruhusu. 
Mungu anatoa tu kibali na tena kile kibali anakitoa kwa kuangalia kiwango chako cha imani. 
Shetani anamwambia Mungu 
"nyosha mkono wako sasa uyaguse yote aliyo nayo uone kama hatakukufuru"
Lakini Mungu anampa shetani hicho kibali cha kwenda kufanya anayoyataka lakini kwa masharti ya kiwango Fulani. 
Hivyo wakati shetani anayafanya hayo ujue na Mungu anakuwepo kutazama asije akavuka mipaka. 

YAKOBO 1:12-13
Heri mtu astahimiliye majaribu; kwa sababu akiisha kukubaliwa ataipokea taji ya uzima, Bwana aliyowaahidia wampendao.

Mtu ajaribiwapo, asiseme, Ninajaribiwa na Mungu; maana Mungu hawezi kujaribiwa na maovu, wala yeye mwenyewe hamjaribu mtu.

*****************

Kama ukiwa mwaminifu kwa Mungu kwa kile unachopitia hakika kitakapoisha hutakuwa MTU wa kawaida. 
Hayo ni mashindano ya Mungu na shetani juu ya imani yako sasa kuwa mwaminifu usije ukampa shetani nafasi ya kujisifu mbele za Mungu. 

Shetani alipoondoka tu mbele za Bwana alifanya uharibifu mkubwa mno kwa AYUBU tena kwa namna ya kumtisha bila kumpumzisha ili ahamaki amtukane Mungu au aiache imani yake ya kumwamini Mungu. 

Mungu anaporuhusu ujaribiwe kwa kiasi Fulani huwa ameshakupima na kuona kwamba unaliweza. 
Na anajuwa kabisa kwamba halitakutisha kwa namna alivyoiona imani yako. 

Kazi inakuwa kwa shetani sasa namna ya kuliandaa ili liwe na utisho mbele ya macho yako wakati litakapokufikia. 

Alifanya mambo mengi kwa wakati mmoja kwaajili ya hasira aliyokuwa nayo ya siku nyingi. 

KWANI SHETANI ALIJUWAJE KAMA AYUBU AMEZINGIRWA NA UKIGO PANDE ZOTE? 

Inamaana kuna siku alienda ili amwangamize akaukuta ule ukigo. 

Kila siku unapokuwa unaomba na kuharibu hizo Kazi za shetani na kumfunua kwa watu wasiozijuwa hila zake halafu wakazijuwa wakaokoka ujue kabisa Ana hasira kubwa sana na wewe. 
Siku ya kujaribiwa kwako ndipo atalipiza lakini kwa masharti ya kiwango cha imani yako na Bwana atakuandalia mlango wa kutokea hivyo wakati huo ni wakati wa kuimba haleluya maana ushindi upo na Mungu yu nawe katika huo wakati. 

AYUBU 1:20-22
Ndipo Ayubu akainuka, akalirarua joho lake, kisha akanyoa kichwa chake, na kuanguka chini, na kusujudia;

Akasema, Mimi nilitoka tumboni mwa mama yangu nili uchi, nami nitarudi tena huko uchi vilevile; BWANA alitoa, na BWANA ametwaa; jina la BWANA na libarikiwe.

Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi, wala hakumwazia Mungu kwa upumbavu.

******************

Kwa mambo yote yaliyomtokea AYUBU wala hakuhangaika kumlaani shetani Bali alimgeukia Mungu na kumshukuru. 

Alisema hivyo vyote nilivipata kwa MUNGU hivyo haviwezi vikachukuliwa na shetani kwahiyo kama vimechukuliwa atakuwa yeye aliyenipa ndiye kachukuwa. 

Angemlaani shetani kama ingekuwa alivipata kwa huyo shetani.

AYUBU 19:25-26
Lakini mimi najua ya kuwa Mteteaji wangu yu hai,Na ya kuwa hatimaye atasimama juu ya nchi.

Na baada ya ngozi yangu kuharibiwa hivi,Lakini, pasipokuwa na mwili wangu nitamwona Mungu;

*****************
Katika majaribu yote hayo AYUBU alijuwa kabisa bado mtetezi wake yu hai na atamtetea tu. 
Tena akamwonyesha tena shetani imani ya ajabu kwamba usijisifu kwa huu mwili uliouharibu hivi maana umesahau kwamba bila huu mwili kuharibika sitaweza kuuvaa mwili mpya na kukaa na Mungu pamoja huku nikimsifu. 

Hii ni imani ambayo hata shetani aliiogopa. 
AYUBU alijuwa kabisa anachopitia ni Kazi ya shetani lakini pia mtetezi wake yupo. 
Haleluyaaa

Alibaki na tumaini moja tu ambalo ni Yesu Kristo katika mitihani yake. 
Hata mke wake mwenyewe alimkana lakini bado alisimama na Mungu


AYUBU 2:9-10
Ndipo mkewe akamwambia, Je! Wewe hata sasa washikamana na utimilifu wako? Umkufuru Mungu, ukafe.

Lakini yeye akamwambia, Wewe wanena kama mmoja wa hao wanawake wapumbavu anenavyo. Je! Tupate mema mkononi mwa Mungu, nasi tusipate na mabaya? Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi kwa midomo yake.

******************

Sasa katika majaribu inabidi umjue sana shetani maana akiona hajafanikiwa kukunasa basi anaweza hata kutumia watu wako wa karibu ili kufanikisha nia yake. 
Ayubu alijuwa kabisa kwamba ikiwa kama Mungu ametaka iwe hivi sasa nitakimbilia wapi? 
Yeye ni Mungu tu hata kama akifanya nini usiikane imani yako. 
Bali mshukuru kwani anakuandalia mema huko mwishoni. 

AYUBU 42:12-15
Basi hivyo BWANA akaubarikia huo mwisho wa Ayubu zaidi ya mwanzo wake; naye alikuwa na kondoo kumi na nne elfu, na ngamia elfu sita, na jozi za ng’ombe elfu, na punda wake elfu.

Tena alikuwa na wana waume saba, na binti watatu.

Akamwita huyo wa kwanza jina lake Yemima; na wa pili akamwita jina lake Kesia; na wa tatu akamwita jina lake Keren-hapuhu.

Katika nchi hiyo yote hawakuwapo wanawake waliokuwa wazuri kama hao wana wa Ayubu; na baba yao akawapa urithi kati ya ndugu zao wana waume.

*****************
HALELUYA HALEYA HALELUYA

Tunaona mwisho wa AYUBU umekuwa mzuri kuliko ule mwanzo wake. 
Je ingekuwaje kama AYUBU angeiacha imani yake na kumkufuru Mungu? 
Faida za AYUBU kushukuru kwa yale mabaya kule mwanzo imekuja kuonekana mwishoni. 

HAKIKA MUNGU WETU ANATUWAZIA MEMA.
AMEEEEEN

NAKUSHUKURU SANA WEWE ULIYEPATA MUDA WA KUFUATILIA MAFUNDISHO HAYA NA UENDELEE KUMTAFAKARI MUNGU NA KULIISHI NENO LAKE KWA JINA LA YESU KRISTO. 
AMEN

#Powered_By_Holly_Spirit

No comments:

Post a Comment