Saturday 28 April 2018

BWANA NI NGOME SIKU YA TAABU

BWANA YESU ASIFIWE

Kwa kusudi na uwezo wa Roho Mtakatifu leo nakuletea somo lenye kichwa kinachosema, 

BWANA NI NGOME SIKU YA TAABU

Hakika Mungu wetu ni mwaminifu na hatamwacha mtu wake aangamie. 

MSINGI WA MAFUNDISHO YETU

NAHUMU 1:7
BWANA ni mwema, ni ngome siku ya taabu; naye huwajua hao wamkimbiliao.

***************

Mungu anaposema kwamba yeye ni ngome siku ya taabu ni kwamba hakuna jambo linaloweza kukutokea hata kama linatisha kiasi gani halafu Mungu asiwepo kukutetea. 

Mungu anajiita yeye ni ngome akimaanisha ni ulinzi mkubwa sana kwako na anakujuwa wewe umkimbiliae siku zote. 
Ikiwa yeye ni mwema basi anakuwazia mema kila wakati hivyo huna haja ya kuogopa maana pale tunakoishia ndiko yeye anakoanzia. 

Yapo mambo magumu sana na ya taabu yanayoweza kukutokea na ukashindwa kujuwa cha kufanya lakini pale tunaposema hapa basi huwa Mungu anaanzia hapo, haleluya. 

DANIELI 3:4-6
Ndipo mpiga mbiu akapiga kelele akisema, Enyi watu wa kabila zote, na taifa, na lugha, mmeamriwa hivi,

wakati mtakapoisikia sauti ya panda, na filimbi, na kinubi, na zeze, na santuri, na zomari, na namna zote za ngoma, lazima kuanguka na kuiabudu sanamu ya dhahabu, mfalme Nebukadreza aliyoisimamisha.

Na kila mtu asiyeanguka na kuabudu atatupwa saa iyo hiyo katika tanuru ya moto uwakao.

****************

Siri ya Mungu kukuonekania siku ya taabu yako ni pale utakapokuwa umemwamini na kumkimbilia yeye. 

Mfalme Nebukadreza alitoa amri ya watu wote kuiabudu sanamu lakini Shedraka na Meshaki na Abednego waliokuwa maliwali huko wilaya ya Babeli walikataa wakamkimbilia Mungu ili awe ngome kwao kwa ile taabu iliyokuwa mbele yao. 
Walikiuka amri ya mfalme na kuamua kumkimbilia Mungu mpaka hatua ya mwisho. 
Halikuwa jambo rahisi sana kama ambavyo watu wanaweza kulichukulia. 

DANIELI 3:14-18
Nebukadreza akajibu, akawaambia, Enyi Shadraka, na Meshaki, na Abednego, je! Ni kwa makusudi  hammtumikii mungu wangu wala kuisujudia sanamu ya dhahabu niliyoisimamisha?

Basi sasa, kama mkiwa tayari wakati mtakapoisikia sauti ya panda, na filimbi, na kinubi, na zeze, na santuri, na zomari, na namna zote za ngoma, kuanguka na kuisujudia sanamu niliyoisimamisha, ni vema; bali msipoisujudia, mtatupwa saa iyo hiyo katika tanuru iwakayo moto; naye ni nani Mungu yule atakayewaokoa ninyi na mikono yangu?

Ndipo Shadraka, na Meshaki, na Abednego, wakajibu, wakamwambia mfalme, Ee Nebukadreza, hamna haja kukujibu katika neno hili.

Kama ni hivyo, Mungu wetu tunayemtumikia aweza kutuokoa na tanuru ile iwakayo moto; naye atatuokoa na mkono wako, Ee mfalme.

Bali kama si hivyo, ujue, Ee mfalme, ya kuwa sisi hatukubali kuitumikia miungu yako, wala kuisujudia hiyo sanamu ya dhahabu uliyoisimamisha.

***********

Mfalme Nebukadreza alitoa tena kauli ya mwisho baada ya kusikia kuwa wamepuuza ile amri. 
Lakini Meshaki na wenzake walimjibu mfalme kwa ujasiri kwamba hatutakubali kuitumikia hiyo miungu yako. 
Na hata kama Mungu wetu hatatutetea hatutakubali kuitumikia hiyo miungu yako. 
Hiyo ndiyo maana ya kumkimbilia Mungu na kumwamini, haleluya. 

Mfalme alikasirika sana kwa majibu yao na akaamuru watupwe kwenye tanuru la moto. 

Kumbuka bado Waliendelea kumwamini Mungu na wakaamini kwamba Mungu wao hashindwi na chochote na waliendelea kumuomba juu ya adhabu iliyokuwa mbele yao. 

DANIELI 3:24-26
Ndipo Nebukadreza akastaajabu, akainuka kwa haraka; akanena, akawaambia mawaziri wake, Je! Hatukutupa watu watatu, hali wamefungwa, katikati ya moto? Wakajibu, wakamwambia mfalme, Kweli, Ee mfalme.

Akajibu, akasema, Tazama, mimi naona watu wanne, nao wamefunguliwa, wanatembea katikati ya moto hali hawana dhara; na sura yake yule wa nne ni mfano wa mwana wa miungu.

Kisha Nebukadreza akaukaribia mdomo wa ile tanuru iliyokuwa inawaka moto. Akanena, akasema, Enyi Shadraka, na Meshaki, na Abednego, watumishi wa Mungu Aliye juu, tokeni, mje huku. Ndipo Shadraka, na Meshaki, na Abednego, wakatoka katika ule moto.

***************

Hapa ndiko shetani huwa anapowatingisha watu wa Mungu imani yao. 
Fikiri ingekuwa ni wewe Mfalme ameahidi kwamba endapo utaendelea kumwabudu Mungu aliye hai atakutupa katika tanuru la moto halafu ukaendelea kumwabudu kwa imani kwamba anaweza kukuokoa usitupwe kwenye hilo tanuru, halafu kadri unavyoomba au kanisa linavyoendelea kuomba juu yako huoni kama kuna tumaini la kushinda ungefanyaje? 

SHETANI ANAKULETEA KUWA NA MASHAKA NA MUNGU WAKO NA HATA UNAWEZA UKAONA HILO NENO LA KUWA BWANA NI NGOME KWAKO NI LA UONGO. 

Labda ni kesi inaendelea mahakamani tena ya kusingiziwa halafu bado wiki moja hukumu isomwe.
Kanisa linaomba na kufunga kwaajili yako lakini badala ya ushindi unashangaa unahukumiwa hata kifungo cha maisha. 
Usipokuwa makini hapo shetani anaweza akakuondolea imani yako. 

Yesu anataka uingie mpaka huko gerezani ili akajitwalie utukufu hukohuko. 
Yesu alimwacha mfalme Nebukadreza awatupe kwenye tanuru ili aonyeshe njia pasipokuwa na njia kabisa kwa akili za kibinadamu. 
Shetani asije akakufanya ukafadhaika kwaajili ya ile hatua mbaya ya mwisho inayoonekana kutokuwa na matumaini kabisa kisha akaipora imani yako.

YOHANA 11:3
Basi wale maumbu wakatuma ujumbe kwake wakisema, Bwana, yeye umpendaye hawezi.

****************
Wakati Lazaro akiwa mgonjwa Yesu mponyaji alipata taarifa zake. 
Na zaidi ya yote biblia inamtambulisha kwamba alikuwa ni rafiki yake. 
Rafiki ni mtu wa karibu sana anayeweza kukusaidia kwa dhati kabisa katika changamoto zako. 
Yesu akishakuwa rafiki kwako hakuna kitakachoshindikana tena. 
Unaweza ukawa na tatizo kubwa mno huku ukiwa wewe ni rafiki yake Yesu yani unaishi kwa misingi yote ya neno la Mungu lakini bado ukaomba juu ya jambo lenyewe halafu ukaona hujibiwi chochote. 

Kama Lazaro pamoja na kuwa rafiki yake Yesu na kumtaarifu kuhusu ugonjwa wake lakini Yesu alinyamaza kimya mpaka mauti yakamkuta. 
Sasa hapo shetani aliingiza mawazo mabaya kwa dada zake Lazaro na kuanza kumlaumu Yesu kwamba angekuwepo wala kaka yao asingekufa. 
Imani yao ilianza kuyumbishwa na kuanza kunung'unika na wakati manung'uniko ni dhambi kwa Mungu na ni kama kumuona Yesu kakosea na wakati huwa yeye hakosei. 
Yesu alinyamaza mpaka Lazaro akafa na akazikwa mpaka mwili kuanza kuharibika. 

YOHANA 11:38-44
Basi Yesu, hali akiugua tena nafsini mwake, akafika kwenye kaburi. Nalo lilikuwa ni pango, na jiwe limewekwa juu yake.

Yesu akasema, Liondoeni jiwe. Martha, dada yake yule aliyefariki, akamwambia, Bwana, ananuka sasa; maana amekuwa maiti siku nne.

Yesu akamwambia, Mimi sikukuambia ya kwamba ukiamini utauona utukufu wa Mungu?

Basi wakaliondoa lile jiwe. Yesu akainua macho yake juu, akasema, Baba, nakushukuru kwa kuwa umenisikia.

Nami nalijua ya kuwa wewe wanisikia sikuzote; lakini kwa ajili ya mkutano huu wanaohudhuria nalisema haya, ili wapate kusadiki kwamba ndiwe uliyenituma.

Naye akiisha kusema hayo, akalia kwa sauti kuu, Lazaro, njoo huku nje.

Akatoka nje yule aliyekufa, amefungwa sanda miguuni na mikononi, na uso wake amefungwa leso. Naye Yesu akawaambia, Mfungueni, mkamwache aende zake.

***************

Yesu alisubiri mpaka siku ya nne maana ilikuwa ni imani ya wayahudi kwamba mtu akifa anaweza akarudi siku ya tatu. 
Walikuwa wanaamini kwamba mtu anapokufa huwa roho yake inakuwa maeneo hayo ikitafuta namna ya kuurudia ule mwili. 
Ndiyo maana Yesu alisubiri mpaka zile siku zao wanazoziamini zipite na waamini kabisa kwamba hapa haiwezekani tena Lazaro kuwa hai kwa namna yoyote ya kibinadamu. 
Yesu anasema kabisa kwamba alifanya hivyo kwaajili ya mkutano ule ili waamini kwamba yeye ni ngome siku ya ile taabu yao. 
Ili waamini kabisa haya yamefanyika kwa Mungu tu na kwa namna ya kibinadamu isingewezekana, BWANA YESU ASIFIWE SANA. 

Sasa usiwe ukawa unamcha Mungu na unapitia katika mambo magumu halafu shetani akaja akakunyang'anya imani yako. 
Endelea kumwamini Mungu. 

UFUNUO 2:9-10
Naijua dhiki yako na umaskini wako, (lakini u tajiri) najua na matukano ya hao wasemao ya kuwa ni Wayahudi, nao sio, bali ni sinagogi la Shetani.

Usiogope mambo yatakayokupata; tazama, huyo Ibilisi atawatupa baadhi yenu gerezani ili mjaribiwe, nanyi mtakuwa na dhiki siku kumi. Uwe mwaminifu hata kufa, nami nitakupa taji ya uzima.

***************

Mungu anakujuwa na yeye ni ngome wakati wa shida yako, 
Endelea kumwamini kama Lazaro alivyoendelea kuamini mpaka mauti na hata alipokufa kila mtu akajuwa hapa habari ya Lazaro imekwisha lakini pale wanadamu walikoishia Yesu akaanzia pale na utukufu wa Mungu ukaonekana. BWANA YESU ASIFIWE SANA.

Shetani anapokuja kwako wakati wa taabu yako huwa anakuja kukunyang'anya imani yako. 
Anakuja kukudanganya kwamba, 
KAMA KWELI MUNGU NI MWEMA NA NI NGOME SIKU YA TAABU NA HUWAJUWA WAMKIMBILIAO NI KWANINI UNAENDELEA KUWA KATIKA WAKATI MGUMU ZAIDI YA JANA? 

Mbona jana ulikuwa afadhali kuliko Leo? Mbona kadri unavyomkimbilia huyo Mungu ndivyo hali inavyozidi kuwa mbaya zaidi? 
LAKINI SHETANI ANAJUWA KABISA UTAKACHOKIPATA NA ATAKAVYOAIBIKA ENDAPO UTAENDELEA KUMWAMINI MUNGU. 

Anakuletea mawazo mengi mengi yote yaliyo kinyume na Mungu tu. 
Anakuletea mawazo ya kutafakari juu ya haja ya moyo wako na jinsi haja hiyo ilivyo kinyume kabisa na wakati unaopitia. 
Unaugua na unatamani ungekuwa mzima, 
Umesingiziwa kesi na unatamani ungeweza kuaminika unachokiongea kuwa ni kweli. 
Usipokuwa makini unaweza kumwona Mungu ni muongo katika neno lake na ukishaamini hivyo ujue tayari imani yako kwa Mungu imeshakwapuliwa. 

YAKOBO 1:14
Lakini kila mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe huku akivutwa na kudanganywa.

***************
Tamaa ya mtu ni jambo analoliona la muhimu sana na linachukuwa nafasi ya pili kutoka Mungu. 
Sasa shetani anaweza kuifanya tamaa yako kuchukuwa nafasi ya Mungu katika maisha yako. 
Ukadhiriki kumwacha Mungu kwa ajili ya ile haja kubwa ya moyo wako. 

Shetani akikuona una imani sana na Mungu wako huwa anakuja kukutikisa wakati wa wewe kujaribiwa na ile tamaa yako. 

Palipo na changamoto yoyote kwako Mungu yuko hapo na shetani pia yuko hapo na ni lazima aje hapo tu maani ni kiherehere sana. 

MWANZO 22:1-2
Ikawa baada ya mambo hayo Mungu alimjaribu Ibrahimu, akamwambia, Ee Ibrahimu! Naye akasema, Mimi hapa.

Akasema, Umchukue mwanao, mwana wako wa pekee, umpendaye, Isaka, ukaende zako mpaka nchi ya Moria, ukamtoe sadaka ya kuteketezwa huko juu ya mlima mmojawapo nitakaokuambia.

**************
Tamaa ya Ibrahimu ya Muda mrefu ilikuwa ni kumpata mtoto na ndiyo maana hata shetani alimjia na kumpa wazo la kuzaa na Hajiri ambapo shetani alipitia kwa mke wake. 
Isaka alikuwa haja ya Ibrahimu siku zote na Ibrahimu akajaribiwa tena kwa mara nyingine kwa ile tamaa yake ya muda mrefu na haja ya moyo wake ambayo ni Isaka mwanaye. 

Lakini shetani alishindwa kuitikisa Imani ya Ibrahimu na hii ni imani kubwa mno kwani Yule mtoto alikuwa na ahadi nyingi sana na ni kama hazina kubwa sana kwa Ibrahimu. 
Ibrahimu hakujali hilo na ndiyo maana ni baba wa imani. 

MWANZO 22:8-13
Ibrahimu akasema, Mungu atajipatia mwana-kondoo kwa hiyo sadaka, mwanangu. Basi wakaendelea wote wawili pamoja.

Wakafika mahali pale alipoambiwa na Mungu, Ibrahimu akajenga madhabahu huko, akaziweka tayari kuni, kisha akamfunga Isaka mwanawe, akamweka juu ya madhabahu, juu ya zile kuni.

Ibrahimu akanyosha mkono wake, akakitwaa kisu ili amchinje mwanawe.

Ndipo malaika wa BWANA akamwita kutoka mbinguni, akasema, Ibrahimu! Ibrahimu! Naye akasema, Mimi hapa.

Akasema, Usimnyoshee kijana mkono wako, wala usimtendee neno; kwa maana sasa ninajua ya kuwa unamcha Mungu, iwapo hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee.

Ibrahimu akainua macho yake, akaangalia, na tazama, kondoo mume yuko nyuma yake, amenaswa pembe zake katika kichaka. Basi Ibrahimu akaenda akamtwaa huyo kondoo, akamtoa awe sadaka ya kuteketezwa badala ya mwanawe.

****************
Ibrahimu alijuwa kabisa kwamba Mungu ni ngome siku ya taabu na ndiyo maana hata Isaka alipomwuliza habari za mwanakondoo alimjibu Mungu atajipatia. 

Mpaka hatua ya mwisho kabisa ambapo Ibrahimu alikuwa amchinje mwanawe na kulikuwa hakuna jinsi nyingine ya kibinadamu Mungu akaanzia pale na utukufu wake ukaonekana, BWANA YESU ASIFIWE SANA. 

SIRI
Mungu hawezi akakubali kuwa ngome kwako wakati wa taabu halafu atokee mtu na miungu yake naye aseme hata hivi alivyofanya Mungu na mimi naweza kufanya na miungu yangu. 
Utukufu wa Mungu hauguswi ni kitu kingine chochote. 

SIFA NA UTUKUFU NI KWAKO MUNGU KWA JINA LA YESU KRISTO. 
NI KWA NEEMA ZAKO TU UMENIFUNULIA HAYA YALIYOSHINDA AKILI NA MAARIFA YOTE YA WANADAMU. 
ASANTE SANA ROHO MTAKATIFU, HAKIKA WEWE NI MWALIMU MWEMA. 
YALELUYA HALELUYA

#Powered_By_Holly_Spirit

Friday 27 April 2018

YESU KRISTO NI YEYE YULE JANA NA LEO NA HATA MILELE.


BWANA YESU ASIFIWE

Leo nakuletea somo lenye kichwa kinachosema, 

YESU KRISTO NI YEYE YULE JANA NA LEO NA HATA MILELE. 

Leo Roho Mtakatifu amekusudia kutufundisha namna ambavyo YESU Kristo alivyo ukomboa huu ulimwengu tangu mwanzo na namna anavyoendelea kuyapigania maisha yetu.
Kuhakikisha kwamba mwanadamu anakuwa huru. 
Hakika sifa na utukufu na heshima na mamlaka vyote ni vya kwake. 

TWENDE KWENYE NENO LETU LA MSINGI

WAEBRANIA 13:8
Yesu Kristo ni yeye yule, jana na leo na hata milele.

**************
Wapo watu wanakuwa na uelewa mdogo kuhusu AGANO LA KALE na AGANO JIPYA kuhusu YESU KRISTO. 
YESU KRISTO hajakuwako katika AGANO JIPYA peke yake. 
Alikuwepo katika MAAGANO yote makubwa mawili.
Bali alijithihirisha waziwazi katika AGANO JIPYA. 

MWANZO 3:21
BWANA Mungu akawafanyia Adamu na mkewe mavazi ya ngozi, akawavika.

**************
Baada ya Adamu kufanya dhambi kwa kula lile tunda ambalo Mungu alimkataza hawakuweza tena kumkaribia Mungu kwaajili ya dhambi hiyo. 
Na pia Mungu hakuweza kuwakaribia kwaajili ya dhambi iliyokuwa mbele yao ya kuwa wa uchi. 

Bwana Mungu aliwafanyia mpango wa kufunika uchi wao ambapo ili kulifanikisha hilo ilibidi Bwana Mungu awafanyie mavazi ya ngozi. 

Tafsiri ya ngozi nyuma yake lazima kuwe na mauti, 
Na nyuma ya mauti lazima kuwepo na kumwaga damu. 
Kuna usemi wa sasa wanasema 
"ukiona manyoya ujue kaliwa. "
Au aliyekamatwa na ngozi ndiye mwizi.
Kwa hiyo hapa tunaona kabisa kwamba, ili mwanadamu huyu aliyetenda dhambi aweze kumkaribia tena Mungu ni lazima damu imwagike. 
Ile damu ya yule mnyama aliyechinjwa na Mungu mwenyewe ndiyo iliyoweza kumkomboa mwanadamu kutoka katika dhambi aliyoifanya. 

WAEBRANIA 10:1-10
Basi torati, kwa kuwa ni kivuli cha mema yatakayokuwa, wala si sura yenyewe ya mambo hayo, kwa dhabihu zile zile wanazozitoa kila mwaka daima, haiwezi wakati wo wote kuwakamilisha wakaribiao.

Kama ndivyo, je! Dhabihu hazingekoma kutolewa; kwa maana waabuduo, wakiisha kusafishwa mara moja, wasingejiona tena kuwa na dhambi?

Lakini katika dhabihu hizo liko kumbukumbu la dhambi kila mwaka.

Maana haiwezekani damu ya mafahali na mbuzi kuondoa dhambi.

Kwa hiyo ajapo ulimwenguni, asema,Dhabihu na toleo hukutaka,Lakini mwili uliniwekea tayari;

Sadaka za kuteketezwa na sadaka za dhambi hukupendezwa nazo;

Ndipo niliposema, Tazama, nimekuja (katika gombo la chuo nimeandikiwa)Niyafanye mapenzi yako, Mungu.

Hapo juu asemapo, Dhabihu na matoleo na sadaka za kuteketezwa na hizo za dhambi hukuzitaka, wala hukupendezwa nazo (zitolewazo kama ilivyoamuru torati),

Ndipo aliposema, Tazama, nimekuja niyafanye mapenzi yako. Aondoa la kwanza, ili kusudi alisimamishe la pili.

Katika mapenzi hayo mmepata utakaso, kwa kutolewa mwili wa Yesu Kristo mara moja tu.

******************
Katika nyakati hizo mwanadamu aliendelea kutakaswa kwa damu ya mafahali na mbuzi, 
Yote hayo yalifanyika lakini Mungu akiyatambua kwamba ni kama kivuli tu cha mambo halisi yajayo. 
Pamoja na Mungu kuchaguwa kwamba njia ya mwanadamu kumwendea anapokuwa na dhambi ni lazima atumie damu lakini ile damu ya wanyama bado aliona kuwa haitoshi kumfanya atakasike na kuwa tayari kuuona uso wa Mungu.
Ndiyo maana Yesu alikuja akaliondoa lile AGANO akasimamisha la kwake ambalo ni la damu isiyo na mawaa, damu isiyoguswa na chochote. 

Mtoto anapokuwa tumboni huwa na damu yake mwenyewe wala damu ya mama haihusiki kivyovyote na damu ya mtoto. 
Damu ya mtoto ni ya mtoto na baba yake, na damu ya mama ni ya mama peke yake.
Ndiyo maana pia mimba ya Maria haikuwa na baba. 
Kama ingekuwa na baba basi Yesu angekuwa na damu yenye uhusiano na damu ya mwanadamu wa kawaida. 
Yesu alizaliwa kama mwanadamu, na kila kitu alifanya kama mwanadamu lakini hakutokana na kizazi cha mwanadamu. 
HIYO NDIYO TOFAUTI KATI YA YESU NA MWANADAMU. 

Wakati wa AGANO LA KALE Yesu alikuwa akijitokeza sehemu mbalimbali kwa kivuli cha damu yake kuokoa, kutakasa na hata kuponya. 

HESABU 21:6-9
BWANA akatuma nyoka za moto kati ya watu, wakawauma, watu wengi wakafa.

Watu wakamwendea Musa, wakasema, Tumefanya dhambi kwa sababu tumemnung’unikia Mungu, na wewe; utuombee kwa BWANA, atuondolee nyoka hawa. Basi Musa akawaombea watu.

Bwana akamwambia Musa, Jifanyie nyoka ya shaba, ukaiweke juu ya mti, na itakuwa kila mtu aliyeumwa, aitazamapo ataishi.

Musa akafanya nyoka ya shaba, akaiweka juu ya mti, hata ikiwa nyoka amemwuma mtu, alipoitazama ile nyoka ya shaba, akaishi.

********************
Hapa tena Yesu alijitokeza kwa sura ambayo hawakuielewa. 
Kwanini Mungu amwambie Musa amtundike huyo nyoka wa shaba? 
Na kweli kila aliyeumwa na nyoka alipoinua macho kumtazama basi aliishi, lakini wapo waliokataa kabisa kumtazama na walikufa. 

YOHANA 3:14-15
Na kama vile Musa alivyomwinua yule nyoka jangwani, vivyo hivyo Mwana wa Adamu hana budi kuinuliwa;

Ili kila mtu aaminiye awe na uzima wa milele katika yeye.

********************
Leo hii wapo watu wenye matatizo na wanaendelea kung'ang'ana dini zao lakini hawamtaki Yesu kabisa wala hawataki kusikia habari ya kuokoka na wanakufa na matitizo ambayo endapo wangekubali kuinua macho juu na kumtazama Yesu pale msalabani wangepona kabisa. 
Mwana wa Adamu aliinuliwa pale msalabani ili kila atakayemwamini na kuinua macho kumtazama awe na uzima wa milele. 

Yesu anaokoa, Yesu anaponya na pia huwafanya watu kuwa huru. 

KUTOKA 12:11-14
Tena mtamla hivi; mtakuwa mmefungwa viuno vyenu, mmevaa viatu vyenu miguuni, na fimbo zenu mikononi mwenu; nanyi mtamla kwa haraka; ni pasaka ya BWANA.

Maana nitapita kati ya nchi ya Misri usiku huo, nami nitawapiga wazaliwa wa kwanza wote katika nchi ya Misri, wa mwanadamu na wa mnyama; nami nitafanya hukumu juu ya miungu yote ya Misri; Mimi ndimi BWANA.

Na ile damu itakuwa ishara kwenu katika zile nyumba mtakazokuwamo; nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu, lisiwapate pigo lo lote likawaharibu, nitakapoipiga nchi ya Misri.

Na siku hii itakuwa ukumbusho kwenu, nanyi mtaifanya iwe sikukuu kwa BWANA; mtaifanya iwe sikukuu katika vizazi vyenu vyote, kwa amri ya milele

******************
Wana wa Israeli walikaa utumwani miaka yote mia nne bila ukombozi wa aina yoyote. 
Tena Musa alivyotumwa na Mungu Farao alikuwa mbishi kuwaachia watu wake. 
Mungu aliipiga Misri kwa mapigo tisa lakini yote yale hayakusaidia wana wa Israeli kuwa huru. 
Kwa mapigo yote tisa hawakujikomboa, hawakupata kuwa huru wala hawakuokoka. 
Lakini hili pigo la kumi ndilo pigo ambalo Yesu Kristo alijitokeza katika sura ya damu na kwa kupitia hiyo damu waliachiwa huru. 
Ishara yoyote katika biblia iliyokuwa na sura ya damu ndani yake kwaajili ya uponyaji, uokoaji au kuweka watu huru ilibeba picha ya Yesu Kristo. 
Kwa kuwa Farao alimshikilia mzaliwa wa kwanza wa Mungu kama alivyomtaja basi Mungu akaachilia mapigo kwa wazaliwa wote wa kwanza wa kila mnyama na mwanadamu katika Misri.
Hakuna nyumba iliyokuwa haina msiba siku hiyo wala hakukuwa na wa kumfariji mwenzie. 
Kwa ile damu wana wa Israeli waliyoipaka kwenye milango ndiyo iliyowakomboa. 
Hapo ndipo ilipoanza PASAKA (PASSOVER) 
Mungu akimaanisha kwamba ata passover (atapita juu) yao atakapoiona ile damu kwenye miimo ya milango yao. 
Na Mungu akaagiza iwe kumbukumbu si sikukuu vizazi vyote.

Tangu wakati wa AGANO LA KALE Yesu aliendelea kufanya ishara na maajabu makubwa kwaajili ya kuwakomboa watu kutoka kwenye utawala wa shetani ibilisi. 

1YOHANE 3:8
Atendaye dhambi ni wa Ibilisi; kwa kuwa Ibilisi hutenda dhambi tangu mwanzo. Kwa kusudi hili Mwana wa Mungu alidhihirishwa, ili azivunje kazi za Ibilisi.

**************
Ibilisi alitenda dhambi tangu mwanzo akiwa hapa ulimwenguni. 
Tangu mwanzo alitenda dhambi kwa kumdanganya HAWA ale lile tunda. 
Mwanadamu akaanza kutawaliwa na dhambi. 
Lakini kwa ile damu iliyomwagika ili kupatikana ngozi ya kumvika mwanadamu kuuficha uchi wake inaonyesha kabisa hata Yesu alikuwa anatenda kazi tangu mwanzo. 
Ila tu hakuwa amedhihirishwa. 
Katika AGANO JIPYA biblia inatuambia, 
"Kwa kusudi hili Mwana wa Mungu alidhihirishwa, ili azivunje kazi za ibilisi."
Hatutakuwa tena wa ibilisi ikiwa amedhihirika kwetu. 

WAEBRANIA 9:15-17
Na kwa sababu hii ni mjumbe wa agano jipya, ili, mauti ikiisha kufanyika kwa kukomboa makosa yaliyokuwa chini ya agano la kwanza, hao walioitwa waipokee ahadi ya urithi wa milele.

Maana agano la urithi lilipo, lazima iwepo mauti yake aliyelifanya.

Kwa maana agano la urithi lina nguvu palipotukia kufa kwa mtu; kwa kuwa halina nguvu kabisa, akiwa yu hai yeye aliyelifanya.

********************
Mauti yake ilifanyika ili tuwe tunatakasiki kwa namna nyingine kabisa ya neema inayodumu. 
Na ilikuwa ni lazima afe ili hilo AGANO JIPYA la damu alilolileta liweze kuwa na nguvu. 
Kama mtu hujafa hata barua za mirathi ulizoziandika kwaajili ya watoto kwamba huyu atarithi hiki na yule atarithi kile hazitaweza kusomwa. 
Siku mtu akifa ndipo zile barua zitakapokuwa na thamani tena kubwa sana. 
Huwezi kusikia kuna kesi ya mirathi mahakamani ikiwa yeye aliye mmiliki wa ile mirathi hajafa. 
Hivyo Yesu alikufa ili hili AGANO JIPYA la damu liwe imara. 

WAKOLOSAI 1:13-17
Naye alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake;

Ambaye katika yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi;

Naye ni mfano wa Mungu asiyeonekana, mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote.

Kwa kuwa katika yeye vitu vyote viliumbwa, vilivyo mbinguni na vilivyo juu ya nchi, vinavyoonekana na visivyoonekana; ikiwa ni vitu vya enzi, au usultani, au enzi, au mamlaka; vitu vyote viliumbwa kwa njia yake, na kwa ajili yake.

Naye amekuwako kabla ya vitu vyote, na vitu vyote hushikana katika yeye.

****************
Alikuja na kudhihirika kwetu kwaajili tu ya msamaha wa dhambi, kumkomboa mwanadamu. 
Na biblia inatuambia kwamba alikuwako kabla ya vitu vyote. 

Katika ile siku ambayo wana wa Israeli waliambiwa kuwa wapake ile damu kwenye miimo ya milango ili wasipate pigo la kuondokewa mzaliwa wa kwanza kwao, ile damu ilikuwa ni kivuli cha damu ya Yesu na ndiyo maana baada ya Yesu kudhihirika kwetu alikuja kujionyesha kwamba ni yeye kwenye kumbukumbu na sikukuu ambayo Mungu aliwaambia waifanya kwa vizazi vyote. 

LUKA 22:19-20
Akatwaa mkate, akashukuru, akaumega, akawapa, akisema, [Huu ndio mwili wangu unaotolewa kwa ajili yenu; fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu.

Kikombe nacho vivyo hivyo baada ya kula; akisema, Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu, inayomwagika kwa ajili yenu.]

*****************
Kama vile wana wa Israeli walivyoambiwa waikumbuke hiyo siku ya pasaka vizazi vyote, 
Ndiyo hivyo hivyo Yesu alivyojidhihirisha katika siku hiyo na kutuambia pia tuendeleze hiyo kumbukumbu. 
Kufa kwake na kufufuka kwake kuliikamilisha maana halisi ya pasaka na kwa kupigwa kwake sisi tumepona. 

Sasa tunao ujasiri wa kupaingia patakatifu kwa damu ya Yesu. 

LUKA 23:44-46
Hapo ilikuwa yapata saa sita, kukawa giza juu ya nchi yote hata saa kenda,

Jua limepungua nuru yake; pazia la hekalu likapasuka katikati.

Yesu akalia kwa sauti kuu, akasema, Ee Baba, mikononi mwako naiweka roho yangu.

*******************
Tulikuwa hatuwezi kuingia kwenye pazia la hekalu ili tukatubu dhambi zetu bila damu lakini kwaajili ya pasaka maana kile kifo chake ni kikombe cha AGANO JIPYA katika damu yake. 

WAEFESO 6:3-8
Hamfahamu ya kuwa sisi sote tuliobatizwa katika Kristo Yesu tulibatizwa katika mauti yake?

Basi tulizikwa pamoja naye kwa njia ya ubatizo katika mauti yake, kusudi kama Kristo alivyofufuka katika wafu kwa njia ya utukufu wa Baba, vivyo hivyo na sisi tuenende katika upya wa uzima.

Kwa maana kama mlivyounganika naye katika mfano wa mauti yake, kadhalika mtaunganika kwa mfano wa kufufuka kwake;

Mkijua neno hili, ya kuwa utu wetu wa kale ulisulibishwa pamoja naye, ili mwili wa dhambi ubatilike, tusitumikie dhambi tena;

Kwa kuwa yeye aliyekufa amehesabiwa haki mbali na dhambi.

Lakini tukiwa tulikufa pamoja na Kristo, twaamini ya kuwa tutaishi pamoja naye;

********************
Tunaweza kuitumia ile damu ya Yesu ikiwa tumetii yote aliyotuagiza, 
Tuliobatizwa katika Kristo Yesu ndiyo tuliokubali kufa naye katika mauti yake na kufufuka naye. 
Wala sisi siyo wafu tena kwaajili ya dhambi ikiwa tumetii yote. 
Yesu anatawala na tunatawala naye kwani kwa njia ya wokovu na ubatizo tulimkiri tukaunganika nanye katika mauti yake, tukafufuka naye na sasa tunatawala naye. 

LUKA 24:47
Na kwamba mataifa yote watahubiriwa kwa jina lake habari ya toba na ondoleo la dhambi, kuanza tangu Yerusalemu.

********************
Yesu Kristo habagui wa kumtakasa, yeyote aliyekubali kumpokea na kufuata njia zake huyo ndiye wa kwake. 
Na ameahidi kuwa yeyote aliyelishika neno lake huyo ndiye wakwake na kamwe hatamwacha. 

MATHAYO 28:18-20
Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.

Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu;

Na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari.

****************
Yesu anataka uyashike yote aliyotufundisha, lakini siyo uamini na kufuata baadhi ya maandiko lakini mengine uyapuuze. 
Mafundisho ya dini za wanadamu na mapokeo yake yasikufanye ukapuuza neno na mafundisho ya kweli ya Kristo Yesu. 
Yeye yuko na sisi mpaka ukamilifu wa dahari. 


ASANTE SANA ROHO MTAKATIFU MAANA WEWE NI MWALIMU MWEMA. 

#Powered_By_Holly_Spirit.

NDOA YENU ILIVYO NI MATOKEO YA MATENDO YENU


BWANA YESU ASIFIWE

Leo nakuletea somo lenye kichwa kinachosema, 

NDOA YENU ILIVYO NI MATOKEO YA MATENDO YENU

Roho mtakatifu kanifundisha hilo somo kwaajili ya baadhi ya mambo ambayo huwa tunamlaumu Mungu lakini wala hatustahili. 

Kila tunachotaka kukifanya huwa tuna mwongozo mzuri sana katika neno la Mungu, 

Na kama tukiufuata huo mwongozo ni lazima tutashinda kwa jina la Yesu Kristo. 

Twende kwenye neno la msingi wa mafundisho yetu. 

ISAYA 48:18

Laiti ungalisikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingalikuwa kama mto wa maji, na haki yako kama mawimbi ya bahari;

*******************

Ukimsikiliza Mungu daima utakuwa mwenye amani juu ya kila majibu ya kila utakachofanya kwasababu utaanza na Mungu na utamaliza na Mungu.

Kamwe hutadhulumiwa haki yako ikiwa unasikiliza amri za Mungu na kutii. 

MFANO

Ni kawaida sana kusikia baadhi ya wanandoa waliooana na kuishi pamoja wakisema kwamba maisha yao yalibadilika na kupoteza amani yote baada tu ya kufunga ndoa.

Hapo utamsikia kila mmoja akimlaumu mwenzake kwamba alikuwa anaficha makucha lakini ukifuatilia maisha yao utagundua siyo kweli na wamefikia hapo walipo kwasababu walimwacha Mungu aliyethibitisha hiyo ndoa. 

Tunaposema wameoana maana yake ni kuendana au kuwa kama sare hiyo ndiyo tafsiri ya kuoana. 

Wale mafundi ujenzi watanielewa nachomaanisha hapa. 

Kama ukikata mbao mwishoni kwa mfano wa herufi "Z" au kimshazari ni lazima mbao nyingine ukate kama hiyo ili zioane utakapounganisha. 

MWANZO 2:18

BWANA Mungu akasema, Si vema huyo mtu awe peke yake, nitamfanyia msaidizi wa kufanana naye.

**************

Ndiyo maana hata Bwana Mungu alilijuwa hilo akamfanyia Adamu wa kufanana naye. 

Kufanana kunakoongelewa hapa siyo sura, umbo au rangi la! 

Kufanana kunakoongelewa hapa ni katika mambo yote. 

Kama uliyenaye hamjafanana na kuoana hamtaoana hata katika tendo la ndoa. 

Kama hamjafanana(hamjaoana) hata mtakapofanya tendo la ndoa mtashangaa mwanamke anakuwa na maumbile madogo na mwanaume maumbile makubwa au mwanaume yanakuwa makubwa na mwanamke madogo mnaishia kuumizana kila siku. 

Hamtaoana hata katika starehe zenu za kawaida. 

AMOSI 3:3

Je! Watu wawili waweza kutembea pamoja, wasipokuwa wamepatana?

****************

Wewe utataka kwenda kaskazini na yeye atataka kwenda kusini kwasababu hamjaoana. 

Yani kila mtakachopanga hamtaweza kuoana katika mawazo yenu. 

Mjue hapo yupo ambaye ameshaenda kinyume na yale makubaliano na viapo mlivyoapa pale madhabahuni

Yupo ambaye hajasikiliza amri za Mungu akafungua mlango adui akaingia.

Ndiyo maana amani hakuna, wala haki yako haitakuwepo.

Ulichopaswa kupewa na mume wako utakitafuta wewe na pia huyo mume naye atakuwa anapata haki yake kwa shetani.

Yani ndiyo pale mwanamke anapofika hatua ya kumkomoa mume wake kwa kumnyima tendo la ndoa ambayo ni haki yake kabisa. 

Mwanaume ataamua kuitafuta hiyo haki kwa Mwanamke mwingine na hapo ndipo tunaposema kuwa ameipata kwa shetani. 

Baraka hazitakuwepo. 

KIAPO

Katika kiapo chochote unachomtaja Mungu lazima Mungu ashuke awepo kuthibitisha. 

MALAKI 2:14
Lakini ninyi mwasema, Ni kwa sababu gani? Ni kwa sababu BWANA amekuwa shahidi kati ya wewe na mke wa ujana wako, uliyemtenda mambo ya hiana, angawa yeye ni mwenzako, na mke wa agano lako.

**************

Sasa usifanye mchezo kabisa katika jambo ambalo Mungu amekuwa shahidi na akaja kuthibitisha maneno yenu mliyoyatamka kwa makubaliano/maagano. 

MWANZO 25:33-34

Yakobo akamwambia, Uniapie kwanza. Naye akamwapia, akamwuzia Yakobo haki yake ya mzaliwa wa kwanza.

Yakobo akampa Esau mkate na chakula cha dengu, naye akala, akanywa, kisha akaondoka, akaenda zake. Hivyo Esau akaidharau haki yake ya mzaliwa wa kwanza.

*****************

Hapa Yakobo anamwambia Esau amwapie kwanza maana alijuwa kabisa kwenye kiapo lazima Mungu wa baba yao wanayemwabudu atashuka kuthibitisha. 

Esau aliondoka akadhani ni kawaida kama vile wanandoa wanavyofunga ndoa wanapanda Madhabahuni mahali patakatifu kisha wanaapa mbele za Mungu kwamba tutakuwa waaminifu, na kupendana halafu baadae uaminifu unavunjwa na mmoja. 

ANGALIA KILICHOMTOKEA ESAU

MWANZO 27:19-29

19 Yakobo akamwambia babaye, Mimi ni Esau, mzaliwa wako wa kwanza, nimefanya kama ulivyoniambia. Ondoka, tafadhali, ukae kitako, ule mawindo yangu, ili roho yako inibariki.

20 Isaka akamwuliza mwanawe, Imekuwaje umepata upesi namna hii, mwanangu? Akasema, Kwa sababu BWANA, Mungu wako, amenifanikisha.

21 Isaka akamwambia Yakobo, Karibu, tafadhali, ili nikupapase, mwanangu, nione kwamba wewe ndiwe mwanangu Esau, ama siyo.

22 Basi Yakobo akamkaribia Isaka, babaye, naye akampapasa, akasema, Sauti ni sauti ya Yakobo, lakini mikono ni mikono ya Esau.

23 Wala hakumtambua, kwa maana mikono yake ilikuwa kama mikono ya Esau, ndugu yake, yenye malaika; basi akambariki.

24 Akamwuliza, Wewe ndiwe kweli mwanangu Esau? Akasema, Ndimi.

25 Akasema, Niletee karibu nami nipate kula mawindo ya mwanangu, ili roho yangu ikubariki. Akamsogezea karibu, naye akala; kisha akamletea mvinyo, akanywa.

26 Isaka, baba yake, akamwambia, Njoo karibu sasa, ukanibusu, mwanangu.

27 Akakaribia akambusu. Naye akasikia harufu ya mavazi yake, akambariki akasema,Tazama, harufu ya mwananguNi kama harufu ya shamba alilolibariki Bwana.

28 Mungu na akupe ya umande wa mbingu,Na ya manono ya nchi,Na wingi wa nafaka na mvinyo.

29 Mataifa na wakutumikieNa makabila wakusujudie,Uwe bwana wa ndugu zako,Na wana wa mama yako na wakusujudie.Atakayekulaani alaaniwe,Na atakayekubariki abarikiwe.

*******************

Unaweza ukafikiri Rebeka na Yakobo walifanya hizi hila au utapeli huu kwa namna ya kawaida lakini ni mpango wa Mungu kabisa na Mungu alitetea haki ya Yakobo kwasababu alikumbuka siku waliyoapa kwa jina lake.

KWANINI MASURIA WENGI WANAISHI KWA AMANI TOFAUTI NA WANANDOA? 

Ni rahisi sana kusikia wanandoa wakilalamika kila mmoja akimlaumu mwenzie kwamba walipokuwa wakiishi pamoja bila ndoa mambo hayakuwa mabaya kama wanavyoishi baada ya kuhalalisha mahusiano yao kwa Mungu kwa njia ya kiapo madhabahuni. 

YOHANA 8:47

Yeye aliye wa Mungu huyasikia maneno ya Mungu; hivyo ninyi hamsikii kwa sababu ninyi si wa Mungu.

***************

Ili mahusiano yoyote ya wanaopendana kwa lengo la kuoana au ya watu wanaoishi pamoja yawe na kibali mbele za Mungu ni lazima myapeleke mbele zake. 

Kama hamjayapeleka mbele za Mungu basi mjue hamjamsikiliza Mungu hivyo ninyi siyo wa Mungu. 

Na kama ninyi si wa Mungu basi ni wa shetani. 

ISAYA 1:19-20

Kama mkikubali na kutii mtakula mema ya nchi;

bali kama mkikataa na kuasi mtaangamizwa kwa upanga; maana kinywa cha BWANA kimenena haya.

****************

Ili mle mema ya nchi kama asemavyo Bwana Mungu ni lazima utii maagizo yake yote aliyoagiza mtekeleze mkiwa wana ndoa mliooana. 

Lakini pia msipomtii Mungu na kusikiliza maagizo yake utakuwa kinyume naye na hapo mtakuwa wa shetani. 

Hivyo mkimtii shetani na kumsikiliza mtakula mema yake ya dunia ambayo ni uharibifu na ni lazima dunia itawanyoosha tu. 

Mema ya shetani mtakayokula ni kama yafuatayo. 

Kama mnaishi miaka yote bila ndoa mtaona kama mna amani ndani yenu kumbe siyo amani bali ni shetani kawatengenezea amani ya uongo. Hakuna amani hapo maana hayo maisha yenu Mungu hajayapa kibali hivyo yameshikiliwa na shetani ambaye katika ufalme wake hana kitu kinachoitwa amani. 

Amani ipo kwa Yesu Kristo tu na ndiye mfalme wa amani. 

Hiyo mnayodhani ni amani mwisho wake ni lazima iwe kilio. 

METHALI 14:12

Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu,Lakini mwisho wake ni njia za mauti.

***************

Shetani anawabembeleza na mnakula mema yake na tena anawajibika ipasavyo maana mmemtii yeye. 

Anapenda sana usaliti na mmoja wenu kuvunja makubaliano mliyowekeana. 

Mmoja akimsaliti mwenzake shetani anajitahidi kumficha huyo mwingine asione ili mzidi kuaminiana na baadaye mfunge ndoa hata kama hamjaoana(hamjafanana) ili tu aharibu lile kusudi la Mungu kwamba

 "akamfanyia msaidizi wa kufanana naye"

Mungu anafunua siri zote lakini shetani hafunui siri.

Yani mlivyokubali kumtii mkaishi bila kufunga ndoa kama atakavyo yeye ataficha maovu ya kila mmoja na siri zake mbaya na chafu ili mridhishane na kujiona waaminifu tena mnaoendana.

Kumbe hamfanani wala hamuoani. 

Ingekuwa nyinyi ni wanandoa mliokula viapo kwamba mtakuwa waaminifu halafu mmoja wenu akatoka nje ni lazima Mungu angefunua hiyo siri kwa mwenzake maana Mungu hafichi uovu. 

LUKA 8:17

Kwa maana hakuna neno lililositirika ambalo halitafunuliwa; wala lililofichwa ambalo halitajulikana na kutokea wazi.

*****************

Hakuna uovu unaofichwa na Mungu ikiwa mlimkabithi mahusiano yenu ayalinde. 

DANIELI 2:22

Yeye hufunua mambo ya fumbo na ya siri; huyajua yaliyo gizani, na nuru hukaa kwake.

*****************

Kama Nuru hukaa kwa Mungu na kweli yote basi ujue giza hukaa kwa shetani na yeye ndiye baba wa uongo. 

Kwahiyo mkishafunga ndoa mtahisi kwamba hayo mambo ni mapya lakini siyo mapya ila yalikuwepo tangu mwanzo na ni shetani alikuwa ameyaficha katika giza lakini sasa kwakuwa mmempa Mungu nafasi yeye anayaweka katika nuru. 

NDOA KAMILI

Mnapofunga ndoa na kula kiapo mbele ya madhabahu ya Mungu mjue kabisa mmoja wenu atakapokiuka kile kiapo ni lazima moto uwake tu. 

Esau alitaka kukiuka kile kiapo lakini Mungu akasema na Rebeka akamwambia haiwezekani maana kuna kitu walishakubaliana tena wakaniita nikathibitisha. 

Mungu hapotezi kumbukumbu. 

Mnakula kiapo kwamba 

"MTAPENDANA KATIKA SHIDA NA RAHA"

"MTAKUWA WAAMINIFU"

Mnapotamka hivyo tu Mungu anagonga mhuri na atakuwa anakiangalia kile kiapo chenu kila siku. 

Kwakuwa mmempa Mungu hilo jukumu la kuwalinda na mkajileta mbele zake basi atawalinda na mtakuwa mnapendana kweli kwakuwa mnamcha BWANA. 

Nasema mtakuwa mnapendana kwakuwa mnamcha BWANA kwasababu. 

KAMA HAKUNA NGUVU YA MUNGU NDANI YAKO HUWEZI KUWA NA UPENDO WA KUJIPENDA WEWE MWENYEWE WALA KUMPENDA MTU MWINGINE. 

Ndiyo maana unakuta mtu ni 

Mlevi, mzinzi, anaendesha gari kwa kasi, anaharibu ngozi yake kwa kujichubua, teja, haogi, anajitesa na njaa bila sababu, nguvu zake zote na jasho lake wanafaidi malaya. 

HUKO KOTE NI KUTOKUJIPENDA NA KUTOKUJUWA THAMANI YAKO. 

Sasa mtu mwenye tabia moja kati ya hizo atasemaje anampenda mtu mwingine ikiwa kujipenda yeye tu ameshindwa? 

Kumpenda mtu mwingine ni neema ya Mungu ila pasipo hiyo neema huwezi kujipenda hata wewe mwenyewe. 

Hivyo usije ukawaona watu wanaishi kwenye mahusiano kinyume na neno la Mungu ukafikiri wanapendana hamna upendo hapo bali ni uongo wa shetani tu. 

Neno linasema kabisa

YOHANA 8:47

Yeye aliye wa Mungu huyasikia maneno ya Mungu; hivyo ninyi hamsikii kwa sababu ninyi si wa Mungu.

******************

Nyinyi siyo wa Mungu mmepata wapi huo upendo? 

Kwani shetani alisema tupendane? 

Mungu atakavyoilinda ndoa aliyoithibitisha na wanandoa wakajiheshimu na kuheshimu kile kiapo huwa shetani anaugua kabisa.

Akiwaona mnaishi kwa msingi wa kile kiapo huwa anakuja kuwajaribu kama kweli mtaendelea kushinda. 

Mtakapoishi kwa misingi ya kile kiapo yani mnapendana na kuwa WAAMINIFU hapo Mungu anaachia baraka zake zinakuja na mtafanikiwa na kuishi kwa furaha maisha yenu yote. 

Shetani anapokuja ili awatikise ili kupima misimamo ya imani yenu huwa anaangalia mlango wa kupitia kwakuwa nyie mmezungushiwa wigo.

YAKOBO 1:14-15

Lakini kila mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe huku akivutwa na kudanganywa.

Halafu ile tamaa ikiisha kuchukua mimba huzaa dhambi, na ile dhambi ikiisha kukomaa huzaa mauti.

***************

Adui akija kwenu wanandoa anakuta mmezungukwa na ulinzi wa Mungu, lakini anachunguza mioyo yenu je, ni yupi naweza kumwingia ili niharibu nyumba nzima? 

Kuna mtu unakuwa umesimama na Mungu lakini kuna kitu fulani huwa ndicho kimekuwa dhambi ya mara kwa mara kwako japo unatubu na kusamehewa lakini unajikuta umerudia tena na tena. 

HIYO NDIYO TAMAA YAKE MTU HUYO. 

Sasa adui anaangalia je wewe baba tamaa YAKO iko wapi au wewe mama tamaa YAKO iko wapi? 

Kama ni kwenye pesa anakukutanisha na mwanaume mwingine mwenye pesa ya kuweza kukushawishi mpaka uzini ili hiyo tamaa ibebe mimba na ikishakomaa izae mauti ya ndoa YAKO. 

Akija kwako baba anaangalia unapenda kitu gani, kama ni wanawake weupe shetani anakupa mzungu kabisa ili uzini na hiyo tamaa ibebe mimba kisha izae mauti ya ndoa YAKO. 

Mnabaki mkijiuliza ni kwanini haya mambo zamani hayakuwepo? Haya mambo yalikuwepo lakini yalijificha kwenye lile giza na uongo wa shetani kwakuwa mlikuwa mnamtii tofauti na sasa ambapo mahusiano yenu YAKO katika ufalme wenye nuru na usioficha maovu. 

Wanandoa mkiishi kinyume na neno la Mungu mtaangamia tu hata iweje. Mungu anafuatilia sana kile kiapo na mtakapokiuka tu mtaangamia. 

Kuna baadhi ya mambo ambayo yakishatokea katika ndoa huwa Mungu anachukizwa nayo sana kiasi cha kugeuka laana katika ndoa na hapo mizozo huanza. 

1PETRO 3:8-9

Neno la mwisho ni hili; mwe na nia moja, wenye kuhurumiana, wenye kupendana kama ndugu, wasikitikivu, wanyenyekevu;

Watu wasiolipa baya kwa baya, au laumu kwa laumu; bali wenye kubariki; kwa sababu hayo ndiyo mliyoitiwa ili mrithi baraka.

*******************

Wanandoa mtakapofanya hayo yote ndipo Mungu atawabariki na mtakula mema ya nchi. 

Lakini mkiacha kushika hata moja kati ya hayo basi mjue kinyume na baraka ni laana iko mbele yenu. 

Mmoja wenu anapofanya jambo tofauti ni adui kapata nafasi ya kuingia ndani lakini bado hajapata nafasi ya kutawala. 

Ili asipate nafasi ya kutawala inatakiwa sasa huyu aliyetendewa aangalie je neno la Mungu linasemaje kwa hili nililofanyiwa? 

WAKOLOSAI 3:12-15

Basi, kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu,

mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama Bwana alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi.

Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu.

Na amani ya Kristo iamue mioyoni mwenu; ndiyo mliyoitiwa katika mwili mmoja; tena iweni watu wa shukrani.

****************

Neno la Mungu linasema amani ya Kristo iamue mioyoni mwenu, na ukiwa na amani ya Kristo ni lazima msameheane, siyo kulipa baya kwa baya bali uushinde ubaya kwa wema. 

UNAPOONA MMOJA WENU AMEFANYA JAMBO LILILO CHUKIZO KWA MWENZAKE BASI UJUE HUYO NI SHETANI KAMWINGIA.

HIVYO ILI UMSHINDE SHETANI UNATAKIWA UTUMIE NGUVU ZA MUNGU AMBAZO ZIKO KATIKA NENO LAKE AMBALO LINASEMA TUSAMEHEANE WALA TUSILAUMIANE. 

Lakini ukisema umshinde shetani kwa kutumia neno la shetani ni lazima dhambi itatawala, shetani atatawala na mwisho ni mauti ya ndoa.

HAYA NDIYO MAKOSA

YEREMIA 31:22

Hata lini utatanga-tanga, Ee binti mwenye kuasi? Kwa maana BWANA ameumba jambo jipya duniani; mwanamke atamlinda mwanamume. 

******************

Mwanamke umeambiwa umlinde Mume wako lakini siyo kwa namna ambayo wanandoa wanalindana kwa sasa kwa kuwindana. 

Yani wanandoa wanaishi wakiwindana na kila mmoja anawaza namna ya kujionyesha kwamba yeye ni mwamba kuliko mwenzake. 

Hayo mashindano ya kuwekeana visasi kiasi hicho Mungu hayafurahii kabisa lazima laana itatawala ndani ya nyumba kwasababu mnaishi nje kabisa ya neno lake.

WAEFESO 5:22-25

Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu.

Kwa maana mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa; naye ni mwokozi wa mwili.

Lakini kama vile Kanisa limtiivyo Kristo vivyo hivyo wake nao wawatii waume zao katika kila jambo.

Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake;

******************

Huwa nikisoma kifungu hiki cha maandiko matakatifu ambayo ni sauti ya Mungu halafu nikiangalia namja ambavyo baadhi ya wanawake wanavyojitahidi kutafuta namna ya kuwa juu ya waume zao ni laana tupu ndiyo maana hata hizi baraka alizoahidi Mungu hazipo kabisa

Nimefanya utafiti maana wapo watu wamenifuata mara nyingi kuniuliza juu ya mahusiano yao yanavyoleta changamoto, pia nikajaribu kuwasikiliza wanawake wanasemaje na wanaume wanasemaje nikapata mawaza tofauti lakini nimegundua kwamba kwa asilimia kubwa hawajajuwa jambo moja tu. 

WAEBRANIA 13:4

Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu. 

******************

Ndoa inahitaji heshima ya kipekee sana na pia kujitambua baina ya wanandoa na majirani na wao kwa wao pia kujitambua kwamba sisi ni watu waliooana. 

Ipo tabia ya zamani ambayo ulikuwa nayo ambayo ni ya kawaida sana ila siyo kwenye ndoa.

Ndoa inahitaji heshima zote.

Tabia zisizooana na tabia za huyo uliyeoana naye achana nazo zitaleta mauti ya ndoa yenu.

Mungu ameshasema ataachilia adhabu endapo utazini na neno la Mungu halipiti bali ni lazima litatimiza mapenzi yake alilolituma. 

Wapo marafiki mnaotakiwa kabisa kuwapa wigo wa mawasiliano yenu, matumizi ya simu zenu ni lazima yawe tofauti na zamani, utani na mazoea na watu wa jinsia tofauti ni lazima msitishe kwani mizaha ni dhambi mbele za Mungu. 

Lazima mwanamke awe chini ya Mwanaume na awe mtii.

Kuwa mtii maana yake ni kutii kila kitu siyo mwanamke kuwa na kiburi.

Kwakuwa wote mpo ndani ya Kristo Yesu wala hakuna haja ya kutomtii mume wako kwa kila kitu kwa kuwa atakayokuelekeza yote yanatoka katika Kristo. 

Kama wewe kijana umeoa na maisha YAKO unayoishi huna tofauti na mtu asiyeoa basi ujue ni lazima dunia ikucharaze tu. 

Kama wewe dada umeolewa na maisha YAKO unayoishi huna tofauti na mtu asiyeolewa basi ujue ni lazima dunia ikucharaze tu. 

Hakuna hila kwa Mungu. 

Utii unapokosekana ndani ya nyumba basi hakuna kitakachoendelea. 

WAFILIPI 2:8

Tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba.

********************

Utii unaoongelewa hapa ni utii haswa ikiwa mpo ndani ya Kristo. 

Mwanamke unapotaka kumtawala mume wako au mume unapoacha kumpenda mke wako basi mjue kuanzia hapo mnatembea kwenye laana. 

Kama kila mmoja akisoma neno na kusimama kwenye nafasi yake kama biblia inavyomuelekeza wala hakuna kitakachopungua. 

Siri ya kushinda majaribu ya ndoa siyo uzuri na urembo wa mke au familia kuwa matajiri bali siri iko katika kuishi ndani ya neno. 

METHALI 31:30

Upendeleo hudanganya, na uzuri ni ubatili;Bali mwanamke amchaye BWANA, ndiye atakayesifiwa.

******************

Mwanamke anayesimama na Mungu ni lazima mume wake amsifu na pia mwanaume anayesimama na Mungu ni lazima mke wake amfurahie. 

Wasichana na vijana wote wa sasa wametekwa na dunia.

Sasa ni bora usijue vitu vyote lakini ujue tu hiki kitakusaidia sana katika maisha yako yote,  kwamba

METHALI 19:14

Nyumba na mali ni urithi apatao mtu kwa babaye;Bali mke mwenye busara, mtu hupewa na BWANA.

******************

Hata kama huyo mke mwema utapewa au mume mwema utapewa na Bwana lakini mkashindwa kuishi kwa kusoma neno basi ni lazima mtaishi kwa kubahatisha tu maana msingi wa wanandoa kuishi ni ni kwa neema ya Mungu na ndiyo maana neno linasema

METHALI 31:30

Upendeleo hudanganya, na uzuri ni ubatili;Bali mwanamke amchaye BWANA, ndiye atakayesifiwa.

********************

Mwanamke amchaye BWANA ndiye atakayesifiwa kwakuwa atakapomcha BWANA ni lazima ataishi na mume wake kwa mwongozo wa neno la Mungu linavyotaka. 

Kila jambo mwezako analokufanyia wewe angalia neno la Mungu linakuelekeza kufanya nini halafu fanya. 

Kama ni kuomba wewe omba na uwe mwaminifu kwa Mungu ni lazima yeye atakutetea. 

Atakufunulia siri usizoamini. 

Lakini cha kushangaza wanandoa wanatumia akili zao wenyewe na wakati ndoa wanayoishi ndani yake ni Mungu aliwapa. 

Tumia akili zako lakini usizitegemee hata kidogo. 

METHALI 3:4-6

Ndivyo utakavyopata kibali na akili nzuri,Mbele za Mungu na mbele ya mwanadamu.

Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote,Wala usizitegemee akili zako mwenyewe;

Katika njia zako zote mkiri yeye,Naye atayanyosha mapito yako.

*******************

Ukimtegemea Mungu ni lazima utawapendeza wanadamu na mbele za Mungu. 

Wanadamu watawasifu na kila mtu atatamani maisha yenu. 

Mtafurahiana na neema ya upendo kwenu itaongezeka pia kila siku itakuwa mpya kwenu na yenye mafanikio makubwa kiroho na kimwili. 

METHALI 31:28-29

Wanawe huondoka na kumwita heri;Mumewe naye humsifu, na kusema,

Binti za watu wengi wamefanya mema,Lakini wewe umewapita wote.

******************

ASANTE SANA ROHO MTAKATIFU MAANA WEWE NI MWALIMU MWEMA. 

SIFA NA UTUKUFU NI KWAKO YESU KRISTO. 

#Powered_By_Holly_Spirit

Thursday 26 April 2018

KATIKATI YA SHIDA UNAYOPITIA MUNGU YUPO

BWANA YESU ASIFIWE

Kwa uweza na nguvu itokayo juu Leo nakuletea somo lenye kichwa kinachosema, 

KATIKATI YA SHIDA UNAYOPITIA MUNGU YUPO. 

Ni kweli kabisa kuna changamoto zinazoweza kukutokea mpaka zikajaribu kuiondoa imani yako. 
Wakati mwingine unaweza ukajaribu hata kumkana Mungu lakini nakuambia hapo hapo ulipo na shida unazoziona bado Mungu amekushika mkono. 

Kwakuwa tu shetani ni baba wa uongo basi anakudanganya kwamba hili jambo haliwezekani ili uiache imani, na zaidi huwa anakutishia juu ya muda na urefu wa kukaa kwa hiyo changamoto ndani yako. 

NENO LA MSINGI

1WATHESOLONIKE 5:18
Shukuruni kwa kila jambo; maana hayo ni mapenzi ya Mungu kwenu katika Kristo Yesu.

*****************
Jambo lolote gumu linapokutokea huna budi kumshukuru Mungu maana mengine ni njia ya kukufikisha katika ndoto zako. 
Lile tatizo ni fursa kwako hivyo inabidi ulifurahie na utazamie ushindi mbele kwa kuwa mwaminifu na Mungu. 

1WAKORINTHO 10:13
Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.

***************
Kwanza utakapopatwa na changamoto amini Mungu ndiye aliyeruhusu hiyo changamoto ije kwako hivyo ni lazima yuko katikati ya hiyo changamoto. 
Mungu ni mwaminifu na ameshasema kwamba hatamuacha shetani akujaribu zaidi ya kiwango cha imani yako. 

Hapo kwenye hilo jaribu Mungu yupo na shetani pia yupo. 
Shetani yupo kwaajili ya kukupepeta akili yako ili ajue kama bado wewe ni wakwake au la. 
Na Mungu anakujuwa kwamba wewe ni wakwake ila tu nae anakuwa pale kumthibiti shetani asije akakutwisha mzigo usio saizi yako halafu akakuiba kutoka katika ufalme wake. 

HIVYO KATIKA SHIDA YAKO MUNGU YUKO KARIBU SANA NA WEWE NA PIA SHETANI YUKO KARIBU SANA NA WEWE. 

Cha kufanya ni wewe kuwa mwaminifu ili Mungu atukuzwe na uwe na ushuhuda uliokamilika kisha akujivunie. 

AYUBU 1:9-12
Ndipo Shetani akamjibu BWANA, na kusema, Je! Huyo Ayubu yuamcha BWANA bure?

Wewe hukumzingira kwa ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo? Kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali yake imeongezeka katika nchi.

Lakini nyosha mkono wako sasa, uyaguse hayo yote aliyo nayo, naye atakukufuru mbele za uso wako.

BWANA akamwambia Shetani, Tazama, yote aliyo nayo yamo katika uwezo wako; lakini usinyoshe mkono wako juu yake yeye mwenyewe. Basi Shetani akatoka mbele za uso wa BWANA.

*****************
Kumbe huwezi kupatwa na changamoto kama Mungu hajaruhusu. 
Mungu anatoa tu kibali na tena kile kibali anakitoa kwa kuangalia kiwango chako cha imani. 
Shetani anamwambia Mungu 
"nyosha mkono wako sasa uyaguse yote aliyo nayo uone kama hatakukufuru"
Lakini Mungu anampa shetani hicho kibali cha kwenda kufanya anayoyataka lakini kwa masharti ya kiwango Fulani. 
Hivyo wakati shetani anayafanya hayo ujue na Mungu anakuwepo kutazama asije akavuka mipaka. 

YAKOBO 1:12-13
Heri mtu astahimiliye majaribu; kwa sababu akiisha kukubaliwa ataipokea taji ya uzima, Bwana aliyowaahidia wampendao.

Mtu ajaribiwapo, asiseme, Ninajaribiwa na Mungu; maana Mungu hawezi kujaribiwa na maovu, wala yeye mwenyewe hamjaribu mtu.

*****************

Kama ukiwa mwaminifu kwa Mungu kwa kile unachopitia hakika kitakapoisha hutakuwa MTU wa kawaida. 
Hayo ni mashindano ya Mungu na shetani juu ya imani yako sasa kuwa mwaminifu usije ukampa shetani nafasi ya kujisifu mbele za Mungu. 

Shetani alipoondoka tu mbele za Bwana alifanya uharibifu mkubwa mno kwa AYUBU tena kwa namna ya kumtisha bila kumpumzisha ili ahamaki amtukane Mungu au aiache imani yake ya kumwamini Mungu. 

Mungu anaporuhusu ujaribiwe kwa kiasi Fulani huwa ameshakupima na kuona kwamba unaliweza. 
Na anajuwa kabisa kwamba halitakutisha kwa namna alivyoiona imani yako. 

Kazi inakuwa kwa shetani sasa namna ya kuliandaa ili liwe na utisho mbele ya macho yako wakati litakapokufikia. 

Alifanya mambo mengi kwa wakati mmoja kwaajili ya hasira aliyokuwa nayo ya siku nyingi. 

KWANI SHETANI ALIJUWAJE KAMA AYUBU AMEZINGIRWA NA UKIGO PANDE ZOTE? 

Inamaana kuna siku alienda ili amwangamize akaukuta ule ukigo. 

Kila siku unapokuwa unaomba na kuharibu hizo Kazi za shetani na kumfunua kwa watu wasiozijuwa hila zake halafu wakazijuwa wakaokoka ujue kabisa Ana hasira kubwa sana na wewe. 
Siku ya kujaribiwa kwako ndipo atalipiza lakini kwa masharti ya kiwango cha imani yako na Bwana atakuandalia mlango wa kutokea hivyo wakati huo ni wakati wa kuimba haleluya maana ushindi upo na Mungu yu nawe katika huo wakati. 

AYUBU 1:20-22
Ndipo Ayubu akainuka, akalirarua joho lake, kisha akanyoa kichwa chake, na kuanguka chini, na kusujudia;

Akasema, Mimi nilitoka tumboni mwa mama yangu nili uchi, nami nitarudi tena huko uchi vilevile; BWANA alitoa, na BWANA ametwaa; jina la BWANA na libarikiwe.

Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi, wala hakumwazia Mungu kwa upumbavu.

******************

Kwa mambo yote yaliyomtokea AYUBU wala hakuhangaika kumlaani shetani Bali alimgeukia Mungu na kumshukuru. 

Alisema hivyo vyote nilivipata kwa MUNGU hivyo haviwezi vikachukuliwa na shetani kwahiyo kama vimechukuliwa atakuwa yeye aliyenipa ndiye kachukuwa. 

Angemlaani shetani kama ingekuwa alivipata kwa huyo shetani.

AYUBU 19:25-26
Lakini mimi najua ya kuwa Mteteaji wangu yu hai,Na ya kuwa hatimaye atasimama juu ya nchi.

Na baada ya ngozi yangu kuharibiwa hivi,Lakini, pasipokuwa na mwili wangu nitamwona Mungu;

*****************
Katika majaribu yote hayo AYUBU alijuwa kabisa bado mtetezi wake yu hai na atamtetea tu. 
Tena akamwonyesha tena shetani imani ya ajabu kwamba usijisifu kwa huu mwili uliouharibu hivi maana umesahau kwamba bila huu mwili kuharibika sitaweza kuuvaa mwili mpya na kukaa na Mungu pamoja huku nikimsifu. 

Hii ni imani ambayo hata shetani aliiogopa. 
AYUBU alijuwa kabisa anachopitia ni Kazi ya shetani lakini pia mtetezi wake yupo. 
Haleluyaaa

Alibaki na tumaini moja tu ambalo ni Yesu Kristo katika mitihani yake. 
Hata mke wake mwenyewe alimkana lakini bado alisimama na Mungu


AYUBU 2:9-10
Ndipo mkewe akamwambia, Je! Wewe hata sasa washikamana na utimilifu wako? Umkufuru Mungu, ukafe.

Lakini yeye akamwambia, Wewe wanena kama mmoja wa hao wanawake wapumbavu anenavyo. Je! Tupate mema mkononi mwa Mungu, nasi tusipate na mabaya? Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi kwa midomo yake.

******************

Sasa katika majaribu inabidi umjue sana shetani maana akiona hajafanikiwa kukunasa basi anaweza hata kutumia watu wako wa karibu ili kufanikisha nia yake. 
Ayubu alijuwa kabisa kwamba ikiwa kama Mungu ametaka iwe hivi sasa nitakimbilia wapi? 
Yeye ni Mungu tu hata kama akifanya nini usiikane imani yako. 
Bali mshukuru kwani anakuandalia mema huko mwishoni. 

AYUBU 42:12-15
Basi hivyo BWANA akaubarikia huo mwisho wa Ayubu zaidi ya mwanzo wake; naye alikuwa na kondoo kumi na nne elfu, na ngamia elfu sita, na jozi za ng’ombe elfu, na punda wake elfu.

Tena alikuwa na wana waume saba, na binti watatu.

Akamwita huyo wa kwanza jina lake Yemima; na wa pili akamwita jina lake Kesia; na wa tatu akamwita jina lake Keren-hapuhu.

Katika nchi hiyo yote hawakuwapo wanawake waliokuwa wazuri kama hao wana wa Ayubu; na baba yao akawapa urithi kati ya ndugu zao wana waume.

*****************
HALELUYA HALEYA HALELUYA

Tunaona mwisho wa AYUBU umekuwa mzuri kuliko ule mwanzo wake. 
Je ingekuwaje kama AYUBU angeiacha imani yake na kumkufuru Mungu? 
Faida za AYUBU kushukuru kwa yale mabaya kule mwanzo imekuja kuonekana mwishoni. 

HAKIKA MUNGU WETU ANATUWAZIA MEMA.
AMEEEEEN

NAKUSHUKURU SANA WEWE ULIYEPATA MUDA WA KUFUATILIA MAFUNDISHO HAYA NA UENDELEE KUMTAFAKARI MUNGU NA KULIISHI NENO LAKE KWA JINA LA YESU KRISTO. 
AMEN

#Powered_By_Holly_Spirit